TIMU MBILI ZAFUTWA NI POLISI TABORA NA GEITA GOLD

Share it:
Boniface Wambura - Mtendaji Mkuu Bodi ya Ligi
  Bodi ya Ligi Tanzania Bara imeziondoa kabisa katika orodha yake timu za Geita Gold Sports na Polisi Tabora kwa kushindwa kuwasilisha usajili wake kwa ajili ya kushiriki ligi daraja la pili msimu huu.
 

Mtendaji Mkuu wa Bodi hiyo Boniface Wambura, amesema maamuzi hayo ni kwa mujibu wa kanuni za bodi hiyo, ambazo haziruhusu timu kushiriki ligi yoyote kama itakuwa haijafanya usajili.

Wambura amesema timu hizo zilishushwa daraja na kutakiwa kushiriki ligi daraja la pili msimu huu, hivyo zilipaswa kuwasilisha majina ya wachezaji wake kwa ajili ya ligi hiyo lakini hazikufanya hivyo hadi sasa, kipindi ambacho ligi imekwishaanza.

"Hatuwezi kuacha kucheza ligi eti kwa sababu wao wana kesi, status waliyonayo ni kucheza ligi daraja la pili, walitakiwa kufanya usajili, sasa kama timu haijafanya usajili, ni timu gani itacheza ligi?, suala la review ya kesi yao siyo wao tu hata Oljoro wanasubiri review lakini walifanya usajili na wanaendelea na ligi" amesema Wambura.
Geita Gold Sports
Kwa upande wa uongozi wa Geita Gold Sports kupitia kwa Seif Kiyunge, amesema wao kama Geita bado hawajapokea taarifa yoyote ya kufutwa, isipokuwa wanachojua ni kuwa hadi sasa wanasubiri rufaa waliyoikata ya kupinga kushushwa daraja isikilizwe, ambapo wanachodai ni mapitio ya hukumu ya awali

"Wasipokuwa makini watalazimika kutulipa pesa nyingi sana maana bado mapitio tuliyoomba hayajafanyiwa kazi, na pia TAKUKURU hawajatoa matokeo ya uchunguzi wa tuhuma za rushwa, kwahiyo endapo itabainika kuwa hapakuwa na upangaji matokeo, na sisi tumeshafutwa itabidi tudai fidia kubwa sana ya kufutwa" Amesema Kiyungi.
Ismail Aden Rage - Mlezi wa Polisi Tabora

Kwa upande wake mlezi wa Polisi Tabora Ismail Rage ametupia lawama Baraza la Michezo kwa kukaa kimya  na kwamba kuna mtu anatakiwa kutumbiliwa kama ilivyokuwa kwa Sepp Blatter wa FIFA.
Share it:

michezo

Post A Comment: