SERIKALI KUPUNGUZA KESI NDOGO NDOGO

Share it:





WAZIRI wa Katiba na Sheria, Dk Harrison Mwakyembe amesema Serikali imedhamiria kupunguza mashauri ya kesi ndogo ndogo ambayo yana watuhumiwa wengi waliojazana magerezani ilhali mashauri yao yangeweza kumalizika kwa muda mfupi.

Aliyasema hayo jana Dar es Salaam wakati alipokutana na kuzungumza na Jaji Mkuu wa Jimbo la Australia ya Kusini nchini Australia, Chris Kourakis.

Alisema uwepo wa mashauri mengi madogo ambayo watuhumiwa wake wanachukua nafasi kubwa kwenye magereza nchini, serikali na mahakama imeona ni eneo lenye changamoto na hivyo linatafutiwa ufumbuzi.

“Hili ni eneo moja ambalo mahakama imeona linahitaji kufanyiwa kazi na liko kwenye maeneo ya ushirikiano baina ya Tanzania na Australia Kusini, kwa sababu yakiangaliwa kwa ukaribu yatapunguza msongamano kwenye magereza yetu na hata kuokoa gharama za kuwatunza,” alisema.

Akizungumzia maeneo ya ushirikiano yaliyoafikiwa kati ya Jaji Kourakis, Jaji Mkuu wa Tanzania, Othman Chande na Msajili Mkuu wa Mahakama, Katarina Revokati, Mwakyembe aliyataja kuwa ni mafunzo na kuwajengea uwezo watumishi wa Mahakama, kuboresha mifumo ya Tehama na kupitia upya Sheria ya Adhabu za Chini.

Akifafanua sheria hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Profesa Sifuni Mchome alisema inaweka kiwango cha chini cha adhabu kwa makosa fulani ambacho hakimu haruhusiwi kutoa adhabu chini ya hapo na kwa baadhi ya makosa.

Jaji Kaurakis alisema nchini Australia, Sheria hiyo ipo na imeweka makosa machache ambayo jaji au hakimu haruhusiwi kutoa adhabu chini ya hapo ili kutoa nafasi ya majadiliano na mtuhumiwa kwa lengo la kutaka mtuhumiwa akubali na kukiri kosa kwa maana ya kujutia alichotenda.
Share it:

habari

Post A Comment: