WANANCHI WAGOMA KUZIKA MWILI WA MAREHEMU WAUTELEKEZA KWA MWENYEKITI WA MTAA

Share it:
Baadhi ya wananchi wakiwa Nyumbani kwa Mwenyekiti wa mtaa wa Nyakabale kata ya Mgusu Wilayani Geita baada ya kuupeleka mwili wa marehemu Zacharia Shabani wakiwadai azike yeye kutokana na kushindwa kutoa ushirikiano baada ya kutafutwa kwa njia ya simu na wananchi hao.

Mzee Yusufu Bangili ambaye ni mkazi wa mtaa wa Nyakabale akielezea namna ambavyo wameendelea kushuhudia Polisi Jamii wakiwapiga wananchi wa mitaa ya Manga na Nyakabale.

Mdogo wa marehemu Bw, Majaliwa Shaban,akizungumza na waandishi wa habari namna ambavyo kaka yake alivyoweza kukutwa na umauti.

Nyumbani kwa marehemu Zacharia Shaban,baadhi ya wananchi wakiwa kwenye hali ya maombolezo.

Mke wa Marehemu,Zacharia Majaliwa ,Bi Leah Joseph akiwa kwenye hali ya maombolezo pamoja  na watoto wake wanne ambao wameachwa na Baba yao.

Wananchi wakiwa wamevunja kibanda kwenye familia ya mwenyekiti wa mtaa wa Nyakabale.

Baadhi ya wananchi wa mtaa wa Nyakabale wakitoka kwa mwenyekiti wa mtaa huo baada ya kuwa wameupeleka Mwili wa Marehemu.


Na,Joel Maduka,Geita.

Baadhi ya Wananchi wa mtaa Nyakabale Kata ya Mgusu  kwenye halmashauri ya mji wa Geita ,wamegoma kuuzika mwili wa Bw ,Zacharia Shaban na kuutelekeza nyumbani kwa Mwenyekiti wa mtaa huo, Bw Elias Ndarawa kwa madai kuwa ameshindwa kutoa ushirikiano na kutoshughulikia tukio  la kupigwa mkazi huyo na polisi jamii hadi kufariki.

Mke wa marehemu Bi Leah Joseph ,alisema mume wake alikwenda kufanya shughuli za utafutaji na kwamba ndani ya siku saba hakuwepo Nyumbani na aliporudi alikuja akiwa na majeraha huku kichwa chake kikiwa kimevimba huku akilalamika kuwa ameumizwa na Polisi jamii na kudai kuwa hawezi kupona kutokana na hali aliyokuwa nayo.

Mdogo wa marehemu Bw, Majaliwa Shaban, alisema tukio hilo lilitokea siku ya jumatatu kwani marehemu alikwenda kuokota mabaki ya mawe ya dhahabu maarufu kwa jina la (MAGWANGALA) kwenye maeneo ya mgodi wa dhahabu wa Geita(GGM) na alikamatwa na kufikishwa polisi ambapo huko amekaa siku sita na baada ya kurudi nyumbani ndipo hali yake ilizidi kuwa mbaya.

Majaliwa aliendelea kusema kuwa walimpeleka hospitali na siku ya Jumamosi Machi 10, 2018 alipoteza maisha akiwa hospitalini kabla ya kupatiwa matibabu na kwamba baada ya kifo walijaribu kumtafuta Mwenyekiti na Mtendaji ambao hata hivyo hawakupokea simu hali iliyosababisha wananchi kubeba mwili na kuupeleka kwa Mwenyekiti.

Bw Mussa Mashauri ambaye ni mkazi wa mtaa huo alisema hawako tayari kuzika hadi serikali itakapotoa kauli kuhusu hatma ya maisha yao na polisi jamii kutokana na namna ambavyo wameendelea kuwapiga na kuwajeruhi.

“Polisi jamii badala ya kutulinda wamekuwa wakitupiga hadi kufikia hatua ya kutudhuru na hilo Mwenyekiti analijua na hajawahi kuingilia kati na kutusaidia na sisi hatujakataa kumstiri ndugu yetu, tunachotaka ni muafaka wa kutuambia ni lini wataacha Polisi jamii kutupiga”Alisema Mussa.

Hata Hivyo mtandao huu ulipotaka kuzungumza na Mwenyekiti wa mtaa huo, Bw Elias Ndarawa aligoma kuzungumzia tukio hilo kwa madai kuwa anaisubiria serikali ndio yenye atoe kauli yake.

Aidha diwani wa Kata ya Mgusu Bw Pastory Ruhusa  alifika  kwenye eneo hilo na kusema kuwa hatua ya wananchi kuutelekeza mwili wa marehemu kwa mwenyekiti sio suala zuri huku akiwataka wananchi kuwa na subira hata kama kuna tatizo na kuachana na tabia  ya  kujichukulia sheria Mkononi.


Kutokana na madai hayo Jana,Machi 11,2018 wananchi walivamia kituo cha Polisi Jamii ambacho kipo mtaa wa Manga na kuvuruga miundo mbinu mbali mbali na kisha kukichoma moto kwenye baadhi ya maeneo.

Share it:

matukio

Post A Comment: